Desemba
6, 2013
TUMEJIANDAA VIZURI KWA MECHI-
TANZANITE
Tanzanite imesema iko vizuri kwa
ajili ya mechi ya mchujo ya Kombe la Dunia kwa wasichana wenye umri chini ya
miaka 20 dhidi ya Afrika Kusini (Basetsana) inayochezwa kesho Jumamosi
(Desemba 7 mwaka huu) Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
Kocha Mkuu wa Tanzanite, Rogasian
Kaijage amesema wamejiandaa vizuri kwa mechi hiyo ya kwanza ya raundi ya pili
itakayochezwa kuanzia saa 10 kamili jioni.
“Tumejiandaa, vijana wako vizuri
wanasubiri saa ya mechi tu. Licha ya kwamba Afrika Kusini wako mbele kwenye
mpira wa miguu wa wanawake si sababu ya matokeo,” amesema Kaijage.
Amesema anaamini vijana wake
watafanya vizuri, na kuwataka Watanzania wajitokeze kwa wingi kuwashangilia
ili waweze kupata matokeo mazuri kwenye mechi hiyo inayotarajiwa kuwa na msisimko
mkubwa.
Naye nahodha wa Tanzanite, Fatuma
Issa amewataka Watanzania kuwaamini kwani wamejipanga kwa ajili ya pambano
hilo, hivyo wawe nyuma yao katika kuwaongezea ari ili waweze kufanya vizuri.
Viingilio katika mechi hiyo ni sh.
1,000 kwa viti vya rangi ya kijani, bluu na orange, sh. 2,000 kwa VIP C, sh.
5,000 kwa VIP B wakati VIP A watalipa sh. 10,000. Tiketi zitauzwa uwanjani
katika magari maalumu.
Mgeni rasmi anatarajiwa kuwa
Waziri wa Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo, Dk. Fenella Mukangara.
RAMBIRAMBI MSIBA WA NELSON MANDELA
Shirikisho la Mpira wa Miguu
Tanzania (TFF) limepokea kwa masikitiko kifo cha Rais wa zamani wa Afrika
Kusini, Nelson Mandela kilichotokea jana (Desemba 5 mwaka huu) nchini humo.
Msiba huo ni mkubwa katika familia
ya mpira wa miguu kwa Afrika Kusini, Afrika na Dunia kwa ujumla kutokana na
mchango mkubwa wa Mzee Mandela katika mchezo huo.
Mzee Mandela anakumbukwa kwa
mchango wake katika Fainali za Afrika (AFCON) zilizofanyika mwaka 1996 nchini
Afrika Kusini na hata zile za Kombe la Dunia zilizofanyika nchini humo mwaka
2010.
TFF tunatoa pole kwa Rais wa Chama
cha Mpira wa Miguu Afrika Kusini (SAFA), Danny Jordan, na wananchi wa Afrika
Kusini na kuwataka kuwa na subira na uvumilivu katika kipindi hiki kigumu cha
msiba huo mzito.
Mungu aiweke roho ya marehemu
Mandela mahali pema peponi. Amina.
Boniface Wambura Mgoyo
Kaimu Katibu Mkuu
Shirikisho la Mpira wa Miguu
Tanzania (TFF)
No comments:
Post a Comment